Thursday, 24 December 2015

Panga la Magufuli lafyeka kigogo Reli


Kasi ya Rais, Dk. John Magufuli, katika kufichua ubadhirifu wa fedha katika taasisi za serikali imeshika kasi ,baada ya jana kumsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli Tanzania (RAHCO), Mhandisi Benhadard Tito.

Kusimamishwa kwa mkurugenzi huyo kumeelezwa ni kupisha uchunguzi  wa kina kutokana na ukiukwaji wa taratibu za manunuzi uliobainika katika mchakato wa utoaji wa zabuni ya ujenzi wa reli ya kati.

Kadhalika, Rais Magufuli amevunja Bodi ya Mamlaka ya Reli Tanzania (TRL), kutokana na kutoridhishwa na jinsi ilivyoshughulikia ripoti ya uchunguzi wa mchakato wa ununuzi wa mabehewa ya treni.

Reli ya kati imekuwa ikilalamikiwa kwa muda mrefu kushindwa kutoa huduma za uhakika kwa wananchi kunakosababishwa na kuharibika mara kwa mara kwa miundombinu.

Kutokana na hali hiyo, Rais Dk. Magufuli katika kampeni zake aliwahi kueleza kuwa atajenga reli hiyo kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge).
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, alieleza kuwa Rais Dk. Magufuli amefikia uamuzi wa kumsimamisha mkurugenzi huyo baada ya kuitisha kikao cha wataalamu kutoka wizara na taasisi mbalimbali za serikali ambazo zinahusika katika utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa yaani ‘Standard Gauge’.

Balozi Sefue alisema  mbali na Rais Dk. Magufuli kumsimamisha kazi mkurugenzi huyo, pia ameivunja Bodi ya RAHCO baada ya kujiridhisha kuwa haikutekeleza ipasavyo wajibu wake katika kusimamia mchakato wa zabuni hiyo na badala yake imeonekana kutetea kilichofanyika.


0 comments:

Post a Comment